Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Riziki Pembe Juma alitaka Jeshi la Polisi Zanzibar kuharakisha masuala ya upelelezi kwa kesi za vitendo vya ukatili na udhalilishaji ili kuona zinamaliza ndani ya muda mfupi.

Posted on: 11.12.2023
Waziri
wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Riziki Pembe Juma amelitaka
Jeshi la Polisi Zanzibar kuharakisha masuala ya upelelezi kwa kesi za vitendo
vya ukatili na udhalilishaji ili kuona zinamaliza ndani ya muda mfupi.
Kauli
hiyo aliitoa jana katika kilele cha maadhimisho ya kufunga siku 16 za harakati
za kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji kwa wanawake na watoto yaliyofanyika
katika kijiji cha Muyuni Wilaya ya Kusini Unguja.
Mhe.
Riziki alisema taarifa za Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
zinaonesha hali inatisha kwani katika kipindi cha mwezi Januari hadi Octoba
2023 jumla ya matukio 1,620 yameripotiwa ambapo matukio 1,360 yanahusu watoto,
194 wanawake na wanaume 77.
Alisema
pamoja na kazi kubwa inayofanywa na Jeshi la Polisi lakini bado ucheleweshwaji
wa upelelezi wa matukio hayo umekuwa mkubwa hali ambayo inapelekea kesi nyingi
kukaa muda mrefu katika vituo vya Polisi Zanzibar.
Alisema
kuendelea kwa hali hiyo itaweza kuathiri malengo ya Serikali katika mapambano ya kuondoa vitendo hivyo pamoja na
kuwatia hatiani watu wanaothibitika kutenda
vitendo vya ukatili na kudhalilisha ndani ya nchi.
Aidha
alisema ipo haja ya kutambua na kuweka kampeni maalum za kuyakabili matendo ya
udhalilishaji wa Kijinsia kwa kuweka nguvu kazi na kampeni isemayo “Wekeza
katika Kuzuwia Ukatili Dhidi ya Watu Wenye Ulemavu” na “Nijuze Nijilinde Dhidi
ya Ukatili wa Kijinsia”.
Alieleza
kwamba kundi hilo la watu wenye ulemavu limekuwa na changamoto kadhaa ambazo
zimekuwa zikiwakabili hivyo haja ya tafakuri ya kina inahitajika katika
kumkomboa mtu mwenye ulemavu dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Mapema
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, bi Abeida Rashid Abdalla, alisema bado matukio ya
udhalilishaji yanaongezeka ikiwemo matukio ya kubaka, kunajisi ambapo Wilaya ya
Mjini na Magharibi ‘A’ na ‘B’ zinaongoza kwa kesi nyingi.
Alieleza
kwamba wakiwa wanahitimisha kilele cha siku 16 lakini bado mapambano
yanaendelea hivyo ni lazima jamii kwa pamoja wanaumme na wanawake wote
wanalazimika kupambana na matendo hayo kwani bado kuna kazi kubwa ya kufanya
ili kuhakikisha matendo hayo yanaondoka nchini.
Naye
Katibu Tawala Mkoa wa Kusini Unguja, bi Radhia Rashid Haroub, aliipongeza Wizara
hiyo kwa kuadhimisha siku 16 za kupinga vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji
katika mkoa huyo. Alisema bado nguvu za
mapambano zinahitajika kwani Mkoa wa Kusini matukio hayo yameongezeka mwaka jana
2022 kulikua na jumla ya matukio 1,320 ambapo kwa mwaka huu yamefikia matukio
1,620 sawa na ongezeko la asilimia 16.
Kwa
upande wa wanaharakati wa kupinga vitendo vya ukatili na udhalilishaji
akizungumza kwaniaba bi Amina Yussuf Ramadhani alisema jamii wameshapata
uwelewa wa kuripoti vitendo hivyo lakini bado tatizo la muhali linaendelea
kujitokeza na kusababisha baadhi ya kesi kusuluhishwa katika ngazi ya familia.